Saturday, July 23, 2016

UTANI WA MTUME NA MASWAHABA ZAKE

Utani wa Mtume swalaLlaahu alayhi wa sallam na maswahaba zake.Utani wa Mtume S.W.A na MASWAHABA ZAKE


Na Dkt. Yusuf Qaradhawi, Mfasiri S. Hussein
Wamisri walianzisha sanaa ya Kafsha ambayo maana yake ni tamathali na taawili ambazo huhusu jambo fulani ili kujenga mazingira ya ucheshi. Watu walikuwa wakitumia kikaragosi cha jadi cha kuchekeshea, Al Aragouz na Khayal Al Zel . Hili ni onesho maarufu la burudani.

Vitendawili au fawazear, ngano au Hawadeat na methali maarufu za kuchangamsha zilikuwa ni sehemu ya burudani za maisha ya kila siku. Njia za burudani ambazo wasanii mashuhuri au mara nyingi watu wasiojulikana majina walizibuni hazikwisha. Burudani hizo ziliendana na mazingira ya wakati huo.

Burudani hizo zilidumu sanjari na pilikapilika za maisha. Zilidhihirisha maadili na mafunzo yaliyoshamiri enzi hizo. Zikabadilika kulingana na mabadiliko ya wakati na mazingira. Kila zama iliacha taathira yake katika burudani hizi.

Dhima ya kila zama  ilikuwa ni kuendeleza burudani za zama za nyuma na kuondosha zile zisizofaa tena. Picha za kuchekesha za katuni ni mfano mmojawapo wa uendelezaji huu. Mara nyingi mimi binafsi nimeulizwa kuhusu fatwa ya Uislamu juu ya vunjambavu, ucheshi na  utani.

Haya mambo ya Kukunja-kunja uso, kununa-nuna, kukasirika-kasirika ambayo kwa kawaida hunasibishwa na watu wenye msimamo mkali wa dini, ndiyo yanayoibua maswali hayo. Hawa huwa hawacheki-cheki na wala hawana utani kiasi kwamba watu huunasibu msimamo huu na Uislamu.

Jawabu langu ni kwamba kucheka ndiko kunakomtofautisha binadamu na jamii nyingine za viumbe. Wanyama hawawezi kucheka kwa sababu kucheka ni matokeo ya ufahamu wa maneno au mambo fulani ya kuchekesha. Kwa kuzingatia hilo, ndio maana mwanadamu huitwa ‘mnyama wa kicheko’.

Ni kweli kabisa kuwa mtu kucheka ndio ubinadamu. Kwa vile Uislamu ni dini ya maumbile, haiwezi kabisa kuzuia utashi wa mtu kucheka na haukatazi mtu kuwa na wasaa wa kufurahi. Kinyume chake, unakikubali kila kitu kinachochangia kuleta furaha na raha ya maisha.

Uislamu unakemea tabia ya kuhuzunika-huzunika na kukata-kata tamaa ya maisha ambayo ndiyo inayomfanya mtu aone kama vile hamna kitu katika sehemu kubwa ya maisha yake

Waislamu hawana budi kufuata nyayo za Mtume ambaye licha ya majukumu mazito aliyokuwa nayo, alikuwa akifanya utani lakini bila kuingiza maneno ya uwongo. Aliishi maisha ya kawaida na Maswahaba wake. Alicheka nao, alifurahi nao na alitaniana nao. Pia alikuwa pamoja nao katika machungu, huzuni na mitihani.

Pale Zaid Ibn Thabit alipoulizwa kuhusu Mtume (saw), alisema hivi: “mimi nilikuwa jirani yake. Wakati wahayi ulipomshukia aliniita na kuniomba niandike aya hizo. Alikuwa pamoja nasi katika furaha zetu. Alikuwa akishiriki katika mazungumzo yetu kuhusu maisha, Akhera na chakula. Nini basi n’takachokwambieni zaidi kuhusu Mtume (saw)?”

Maswahaba wake walimuelezea kama ni mmoja wa watu wacheshi mno. Akiwa nyumbani, alikuwa alitaniana na kufurahishana na wake zake. Alikuwa hata akisikiliza hadithi (ngano) zao kama alivyosimulia Umu Zahara katika Hadith mashuhuri ndani ya Sahihi Bukhari.

Ilisimuliwa kuwa Mtume alikuwa akiinama ili wajukuu zake Hassan na Hussein wapande mgongoni mwake. Hakuona aibu wala hakujisikia vibaya pale mmoja wa Maswahaba zake alipomuona na wajukuu zake mgongoni mwake. Swahaba huyo aliposema: “nyie mnapanda mgongo wa mbora wa watu wote.” Mtume akasema: “hawa ni wabora wa wapandaji wote!”

Imesimuliwa kuwa Mtume alimtania bi mkubwa mmoja ambaye alisema: “Ewe Mtume wa MwenyeziMungu! Niombee kwa MwenyeziMungu ili Aniidhinishe kuingia Peponi. Mtume akasema: “O swahabati wangu we, hakuna mwanamke mzee atakayeingia Peponi!” Bi mkubwa alipoanza kulia kwa sababu ya kuelewa vibaya maneno ya Mtume, Mtume akambembeleza akisema kuwa yeye alikuwa na maana kuwa (yeye bi mkubwa) ataingia peponi akiwa mwali mbichi kabisa na sio mzee kama vile alivyokuwa. Akasoma aya hii:

“Tutawaumba kwa umbo (bora zaidi) na tutawafanya vijana kama kwamba
ndio kwanza wanaolewa.” (56:35-36).

Ilisimuliwa kuwa mtu mmoja alimuomba Mtume ampatie kipando. Mtume
(saw) akasema: “nitakupatia mtoto wa ngamia jike.” Mtu huyo
akayachukulia maneno hayo kwa uzito wake na kusema: “Ewe Mtume wa
MwenyeziMungu, nitamfanyia nini mtoto wa ngamia jike”? Mtume
Akafafanua,  hivi jamani sio ngamia majike wanaozaa ngamia wote*

Maana ya maneno haya ni kwamba mtoto kwa mama hakui, hata akiwa mkubwa huitwa mtoto wa mama fulani. Mtume aliposema mtoto wa ngamia, alikuwa na maana kwamba ngamia huyo si lazima awe ndama. Kinachosemwa tu ni kwamba huyo mtoto wa ngamia hata kama naye ni mkubwa lakini bado kazaliwa na ngamia jike, kwa hiyo ni  mtoto wa ngamia jike-(ufafanuzi wa Mfasiri)

Zaid ibn Aslam kasimulia kuwa mwanamke mmoja aliyeitwa Umu Ayman
alikuja kwa Mtume na kusema: “Mume wangu anataka kukuona.” Mtume
akasema kwa utani: “Ni nani huyo/ ana weupe-weupe hivi ndani ya jicho
lake?” Mwanamke huyo akasema: “Wallah hapana! Hana weupe jichoni
mwake!”

 Mtume akasema, “mimi nakuhakikishia kuwa anao weupe
 jichoni   mwake.” Mwanamke huyo akasema tena: “O hapana Wallah.”
Mtume akafafanua, “hakuna mtu asiye na weupe jichoni mwake. Mtume
hapa alikuwa na maana ya ile sehemu inayozunguuka duara la ndani
 ya jicho. (Kwa hiyo Mtume alikuwa anamtania tu kwani hakuna binadamu
 asiye na ngozi nyeupe ya ndani ya jicho).

Anas Bin Malik kasimulia: “Mtume (saw) alikuwa akichanganyika nasi kiasi
ambacho alipata kumwambia mdogo wangu mmoja wa kiume mdogo sana:
“Ewe baba Umair! Kafanya nini Nughair (ndege wa aina fulani)?”

Aisha (ra) kasimulia: Mtume wa MwenyeziMungu na Sauda Bint Zamaa
walikuwa nyumbani kwangu, nami nikapika Hareera-unga wa kupika na
maziwa na mafuta. Nikawapa chakula na kumwambia Sauda, ‘Endelea
kula’. Akasema, “mimi sipendi chakula hiki’. Nikamwambia: ‘Wallah
utakula chakula hiki, la sivyo, nitakusiliba na chakula hiki usoni. Akasema
‘tena sitakionja hata kidogo.’ Basi nikachukua kiasi cha chakula kwenye
sahani na kumsiliba nacho usoni huku Mtume (saw) akiwa amekaa katikati
yetu.Mtume akashusha chini magoti yake aliyokuwa ameyakunja ili Sauda
aweze  kunivaa vizuri. Hivyo, na yeye akachukua kiasi cha chakula na
kunisiliba nacho usoni. Mtume akasimama hapo hapo akicheka.’

Ilisimuliwa kuwa Ad Dahak Ibn Sufyan Al Kalabi alikuwa mtu mwenye
 sura mbaya. Pale Mtume (saw) alipopokea kiapo chake cha utii,
alimwambia mtu huyo: “Mimi nina wake wawili ambao wanakufaa zaidi
kuliko huyu Humayraa-mwanamke mwenye mashavu ya kahawia-bila shaka
tukio hili lilitokea kabla ya Aya iliyofaradhisha kuteremsha shungi.
 Mtume akaendelea kusema, ‘nakusudia kumtaliki mmoja wao ili umuoe
wewe!’ Aisha alikaa akisikiliza kisha, hatimaye akasema : ‘Hivi mwanamke
huyo ni mbora kuliko wewe au wewe ndio mbora?” Mtume akasema, “mimi
ni mbora na mtukufu zaidi kuliko yeye.’ Mtume akacheka kwa ujanja wa
Aisha wa kuuliza swali la kupiga chenga kwani bwana huyo alikuwa mbaya
wa sura.”

Mtume (saw) alizipenda sana nyakati za kushereheka kama vile sikukuu za
Idd na sherehe za harusi. Wakati Abu Bakr (r.a) alipoonesha kuchukizwa na
nyimbo za waimbaji wawili wa kike nyumbani kwa Mtume (saw) katika
sikukuu na kuwakaripia, Mtume (saw) akasema: ‘Ewe Abu Bakr! Waache
waimbe kwani hii ni sikukuu’. Katika kauli nyingine, alisema: ‘Ili Wayahudi
wajue kuwa sisi tuko huru katika dini yetu.”

Mtume  alimruhusu Aisha aone onesho la Wahabeshi ambao walikuwa
wakicheza na ngao na mikuki katika sikukuu ya Idd. Alimuwezesha
kusimama nyuma yake na kutazama onesho lao Msikitini. Mtume
aliwahamasisha watumbuizaji hao: “Endeleeni! Enyi Bani Arfida.”

Sina budi kusisitiza kuwa Mtume hakuonesha ishara yoyote ya kukataa au
kukerwa na jambo hili. Mtume alielezea kutofurahia kwake kusherehekea
harusi bila burudani au kuimba. Alimwambia Aisha: ‘Ewe Aisha! Je
hukupata burudani yoyote wakati wa sherehe ya Harusi kwani Ansari
hupenda burudani? Katika kauli nyingine, alisema, “ungewapeleka
wasichana wa kuimba pamoja naye (bi harusi) ili wamwimbie mwimbo
 huu:‘Sisi tuko hapa kwa ajili yako Tusabahi, tukusabahi’.

Maswahaba wa Mtume na wale waliowafuata walikuwa wakicheka na
 kutania. Mtume alitoa mfano bora wa mafunzo kwao. Ilisimuliwa kuwa
Umar Ibn Khattab ambaye alijulikana kwa ukali na ugumu alitaniana na
mjakazi wake akisema:

 ‘Muumba wa watu wema ndiye aliyeniumba mimi na Muumba wa watu
waovu ndiye aliyekuumba wewe.’ Umar alipoona kuwa mjakazi huyo
kafadhaika, akafafanua, “MwenyeziMungu ndiye Muumba wa wote , wema
na waovu.”

Baadhi ya Maswahaba walifahamika kwa tabia ya kuchekesha-chekesha,
utanani-utani, licha ya hivyo, Mtume (saw) hakukataza jambo hilo. Hata
baada ya kutawafu kwa Mtume (saw), Maswahaba hawakutamka kulipinga
 jambo hilo.

Katika nukta hii, sina budi kushadidia baadhi ya matukio ambayo tabia hii
ya utani iliachwa huru, lau matukio hayo yangelitokea hivi leo, basi
yangepingwa vikali na wahafidhina wengi ambapo watu hao wenye tabia ya
utani-utani wangelaaniwa kuwa ni Waislamu waliopotea na kupoteza dira la
ukweli.

Annuayman Ibn Umar Al Ansar alifahamika sana kwa tabia ya ucheshi na
uchangamfu. Ilisimuliwa kuwa alikuwa na aina ya pekee ya ucheshi. Bwana
 huyu alishuhudia kiapo cha Akaba, Badr, Uhd, Handaki na vita vingine
.Zubair Ibn Bakar, katika kitabu chake kiitwacho, ‘Ucheshi na Vichekesho,’
kasimulia baadhi ya matukio ya kuchekesha ya Bwana huyo. Mathalani:
Wakati wowote alipoingia Madina alikuwa akinnunua kitu hata kama
alikuwa hakupanga kukaa huko muda mrefu kisha akaenda kwa Mtume
(saw) na kusema: ‘Hii ni zawadi yangu kwako. Pale muuzaji alipokuja kudai
 hela, akampeleka kwa Mtume (saw) na kumwambia: ‘mpe huyu bwana hela
ya vitu vyake.’ Mtume alipokataa akisema: ‘lakini hii si  ilikuwa zawadi
kutoka kwako?’ Bwana huyo akasema: ‘Wallah, sikuwa na hela kununulia.
 Nilitaka tu wewe ule kitu hiki. Basi Mtume akacheka na kumpa muuzaji
hela yake.

0 comments:

Post a Comment

MWEZI WA MUHARRAAM NA UZUSHI

بسم الله الرحمن الرحيم MASHIA NA BIDAA ZA MWEZI WA MUHARRAMU. Mwezi wa Muharramu ni miongoni mwa miezi mitukufu kwa mujibu wa mafundis...